NAIBU Waziri wa Uchukuzi, Charles Tizeba, amewataka mafundi upande wa Reli ya Tanzania na Zambia (TAZARA), kuhakikisha wanakamilisha kwa wakati Mradi wa Treni za mijini kama walivyokubaliana na serikali na si vinginevyo.
Akizungumza na wandishi wa habari jijini Dar es Salaam jana, wakati wa ziara ya kushtukiza katika kuangalia ukarabati huo, Tizeba, alisema ameridhishwa na juhudi za mafundi wa Shirika la Reli Tanzania (TRL), ambako ndiko alikoazia ziara hiyo.
Alisema kutokamilika kwa mradi huo kutazua maswali mengi kutoka kwa wananchi,kwa sababu wanausubiri kwa hamu mradi huo ambao una lengo la kuwapunguzia adha ya msongamano wa magari jijini.
Aidha, alisema kuwa hatawavumilia na kuwaamini mafundi hao kutokana na utaratibu mbovu wa utendaji kazi.
“Tumewaahidi watanzania kuwa hadi Oktoba mwaka huu mradi utakuwa umekamiliaka, wakati leo hii hamjakamilisha hata robo ya kazi”alisema Tizeba.
Akitoa onyo, Tizeba alisema kutokamilika kwa mradi huo wafanyakazi hao watambuwe kuwa wataingia matatani na Watanzania.
Akizungumzia kuhusu mafundi wa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRL), alisema kwa kiasi kikubwa wamejitahidi, na itakapofika Septemba 15 mwaka huu mabehewa sita yataanza kazi kwa majaribio kuanzia Ubungo hadi bandarini.
Vilevile alisema anatoa nafasi kwa mafundi hao kuangalia uwezekano wa kuuziana kazi ikiwa ni kuongeza malipo kwa wafanyakazi na vibarua wao ,lengo likiwa ni kuongeza kasi ya utendaji kazi na kukamilisha mradi huo kwa haraka.
“Huu mzigo tuliojitwisha ni mzito na hii ni kutokana na ahadi tulizo waahidi watanzania kuwa mradi huu utakamilika haraka na safari kuanza mara moja”alisema.
Tizeba alisema mradi huo utakapokamilika anaamini kuwa utasaidia katika kuimalisha uchumi wa nchi ambao tayari umesimama kutokana na changamoto ya foleni za magari jijini.









