Marehemu Daudi Mwangosi enzi za uhai wake.
…………………………………………….
NA MWANDISHI WETU – MAELEZO
WAZIRI wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Dk. Emmanuel Nchimbi amesema askari anayetuhumiwa kusababisha kifo cha aliyekuwa mwandishi wa habari wa kituo cha televisheni cha Channel 10, marehemu Daudi Mwangosi amefikishwa mahakamani leo.
Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa na wizara hiyo iliyosainiwa na Waziri Nchimbi ilieleza kwamba Septemba 7,mwaka huu alikabidhiwa taarifa ya awali ya uchunguzi wa polisi juu ya kifo cha mwandishi huyo na Mkuu wa Jeshi la Polisi, Inspekta Jenerali Said Mwema.
Hivyo Septemba 11, mwaka huu aliliagiza Jeshi la Polisi kumpeleka mtuhumiwa huyo askari namba G. 2573 PC Pasifious mahakamani leo kama ilivyotakiwa ma Mkurugenzi wa Mshtaka(DPP).
Waziri Nchimbi alisema wakati mtuhumiwa huyo amefikishwa mahakamani , kamati iliyoundwa chini ya Jaji Ihema itaendelea na kazi yake ili kupata suluhisho la kudumu la migongano ya kikazi kati ya polisi na waandishi wa habari na waandishi wa habari, polisi na vyama vya siasa ikiwemo kuboresha mahusiano zaidi kati ya polisi na raia.
Aliongeza kuwa mkondo wa sheria umeanza kufuatwa nawaomba wadau wote kutoa nafasi kwa utaratibu huo wa kisheria kufanya kazi.
Aidha aliongeza kuwa uchunguzi huo wa awali ulibaini mambo makubwa mawili ,ambayo ni mlipuko uliotokea ulitokana na bomu la Machozi na bomu hilo lilifyatuliwa na askari huyo.




